UTENZI WA MWANA KWETU
1. Namshukuru manani,
Mola
mwingi wa hisani,
Kanileta
kwenye fani,
Ingawa
nachechemea.
2. Napoitazama
kesho,
Huwa
lanitoka jasho,
Mwili
washika muasho,
Nabaki
najikwangua.
3. Kisha
natazama mbali,
Kwa macho yangu mawili,
Ninamuona batuli,
Mwanakwetu asogea.
4.
Mwanakwetu ni mrembo,
Amejaaliwa umbo,
Yampendeza mapambo,
Macho yake yavutia,
5.
Mwanakwetu ni kiziwi,
Ahofu
kuchoma biwi,
Kelele kwake haziwi,
Aweza kuvumilia.
6. Mwana
kwetu ni kipofu,
Alo
na mema sufufu,
Kamjalia
latifu,
Vipawa
vyake mamia.
7. Mwanakwetu pia bubu,
Kichwa
chake ni dhahabu,
Amekusanya
vitabu,
Vizuri
kapangilia.
8. Mwanakwetu ndiye dada,
Wa
mjombae Akida,
Alimlipia
ada,
Elimu
kuiendea.
9. Anazijua kanuni,
Vifungu
vipo kichwani,
Vyeti
amejaza ndani,
Kwa
kanuni kusomea.
10. Hana mwili wa kushiba,
Lakini
nguvu si haba,
Anaishinda
mibaba,
Ulingoni
Kiingia.
11. Ukoo ulotukuka,
Ukampa
madaraka,
Akaja
vuka mipaka,
Kijijini
kaingia.
12. Nguli muwajibikaji,
Sio
mbabaishaji,
Wakamvisha
mataji,
Sifa
kummiminia.
13. Alisimama kidete,
Ya
nyumbani wasitete,
Lakini
chuma ulete,
Alishindwa
kuzuia.
14. Walimtisha wababe,
Wale
wapigao debe,
Eti
wamkate ngebe,
Vitisho
wakamtia.
15. Akawafata manunda,
Kama
somo kuwafunda,
Kwa
shukurani ya punda,
Mbio
wakamtimua.
16. Wakamchimbia shimo,
Aje
azamie humo,
Hakikutosha
kipimo,
Hadi
ng’ambo akatua.
17. Alingoja barazani,
Ili
apate idhini,
Kuingia
sebuleni,
Apokuja
kutembea.
18 Mwanakwetu si mpweke,
Yupo
kwenye ndoa yake,
Mume
na watoto wake,
Wote
awaheshimia.
19. Walojifanya vidume,
Ndo
wakaja shime shime,
Ukawarusha
umeme,
Kitu
hawakuambua.
20. Ulipozidi uasi,
Likamshinda
nanasi,
Kwa
wingi wa ukakasi,
Chini
akaliachia.
21. Mwanakwetu amerudi,
Ameliacha
baridi,
Kasamehe
zumaridi,
Nyumbani
amerejea.
22. Amekiacha kijiji,
Bado
kinamhitaji,
Kwa
wake wingi umbuji,
Huko
wanamlilia.
23. Moyo wangu hautangi,
Bali
furaha kwa wingi,
Mwanakwetu
si shangingi,
Tija
tutajipatia.
24. Si sahiba wa zarambo,
Si
mchafuzi wa mambo,
Anasa
si lake pambo,
Kwayo
hajapta ngoa.
25. Nyumbani kwetu
pachungu,
Imekithiri
mizungu,
Umezagaa
ukungu,
Wajibanza kudokoa.
26. Kuna pitu na pituzi,
Wametega
shambulizi,
Kwa
yeyote mdakuzi,
Humo
atatumbukia.
27. Walumbi wa utatuzi ,
Wapo
chini ya wabezi,
Sauti
hawazipazi,
Nyaya
wamewakatia.
28. Watendao ya husuni,
Eti
ndio wahaini,
Na
wajazao batini,
Hao
twawanyenyekea.
29. Hawajali ya adili,
Wengi
wao majahili,
Wamezoea
batili,
Ndio
iliyowalea.
30. Aheshimika bahau,
Atuletea
balau,
Twashiba
twajisahau,
Twashindwa
kuzingatia.
31. Wametuwekea chambo,
Tukanasa
kwa ulimbo,
Wakapiga
kingorimbo,
Mali
waje kuchukua.
32. Nyumba imekua gofu,
Ni
zizi la wahalifu,
Wenye
madhambi sufufu,
Ndani
wanakimbilia.
33. Baba kuoa mitala,
Akashikwa
na halala,
Kikamshinda
chakula,
Mauti
yakamjia.
34. Wana wa mke mkubwa,
Ndio
kina bwana Ubwa,
Wanajilia
ubwabwa,
Wengine
wakodolea.
35. Wana wa mke mdogo,
Ikawachosha
mikogo,
Wakawatupia
kago,
Jeuri
yao kung’oa.
36. Siku zinazidi kwenda,
Kago
lazidi kutanda,
Puresha
nayo yapanda,
Kisasi
kikaingia.
37. Sifa yetu ya amani,
Sasa
ipo mashakani,
Udugu
wetu tabani,
Mashine
wapumulia.
38. Wanoleta pingamizi,
Wamesambaza
kutuzi,
Japo
nao mabazazi,
Kinai
imewafaa.
39. Sioni Kwao azizi,
Watosita
kutuhizi,
Umaliki
wakihozi,
Tabuni
tutaingia.
40. Nakeshea matilaba,
Kwa
ghubari la ghiliba,
Lisibaki
hata haba,
Balaa
sije tunyea.
41. Kwa kunuti za uturi,
Zikanijibu
sayari,
Tumeishusha
johari,
Mwanakwetu
kutatua.
42. Tumemuongeza ari,
Tumempa
ujasiri,
Kuliondoa
ghubari,
Ghiliba
kutokomea.
43. Katika waadilifu,
Mwanakwetu
maradufu,
Hawezi
kula nyamafu,
Mbali
ataitupia.
44. Amezunguka kitambo,
Katika
nchi za ng’ambo,
Anakijua
kimombo,
Vigumu
kumpindua.
45. Wale wanusao shombo,
Wakasogeza
matumbo,
Atawachapa
kwa fimbo,
Uchu
wataujutia.
46. Atakuja panda mbegu,
Zirudishazo
udugu,
Ataondoa
magugu,
Jinale
atatumia.
47. Karibia Mwanakwetu,
Roho
zetu zipo kwatu,
Kukupokea
mwenzetu,
Uje
kutupigania.
48. Na wako uanamama,
Tunakupa
taadhima,
Mbele
yetu kusimama,
Amri
kutupatia.
49. Vichwa chini twainama,
Twaja
kwako kuungama,
Tuko
na wewe daima,
Kwa
raha na shida pia.
50. Tutakua watiifu,
Juu
yako Mtukufu,
Na
atayekukashifu,
Vita
tamtangazia.
51. Nami ninakupa rai,
Milikiyo
iwe hai,
Simuige
kibwangai,
Alipokatwa
mkia.
52. Alipoacha unyani,
Kasaliti
masikani,
Japo
walimuamini,
Aende
kuwachumia.
53. Isikushike zohali,
Ikufanye
utudhili,
Kuongeza
tamthili,
Ya
waliotangulia.
54. Usije vaa libasi,
Kinyume
Navyonakisi,
Yakatokea
maasi,
Hatari
kupindukia.
55. Nyumba itajaa damu,
Si
dokita si hakimu,
Atakwenda
kuhudumu,
Nyumba
itaangamia.
56. Watakimbia wageni,
Kurudi
ughaibuni,
Hakutabaki
mjini,
Wala
vijiji kumea.
57. Usiwe na ndimi mbili,
Umuogope
Jalali,
Uiepuke
aili,
Mana
kago Kujitia.
58 Mweledi kima cha konzi,
Inapasa
Kumuenzi,
Mwalimu
na mwanagenzi,
Pasiwe
wa kubagua.
59. Uwafanye mahabubu,
Viziwi
nao mabubu,
Sisite
kuwaadhibu,
Hadhi
wanowashushia.
60. Si amue peke yako,
Washirikishe
wenzako,
Mawazo
yao na yako,
Jema
litapata njia.
61. Barazani weka jamvi,
Vijana
na wenye mvi,
Mwenye
kuongeza chumvi,
Sisite
kumtimua.
62. Mwanakwetu niridhie,
Karatasi
kachukue,
Mtini
uning’inie,
Matunda
kutuchumia.
63. Debe nitakupigia,
Kwa
tenzi za kuvutia,
Senti
sitatarajia,
Lengo
hili kutimia.
64. Kwa uzani wa ratili,
Unawazidi
kwa mbali,
Naona
kila dalili,
Kileleni
tafikia.
65. Kila pande nitapita,
Nikipiga
tarumbeta,
Niwaondoe
matata,
Waje
kukushangilia.
66. Usingizi sitapata,
Mdomo
sitaufyata,
Hadi
uweze kupita,
Ikiwa
salama njia.
67. Chochote sitapurura,
Kuharibu
yako sura,
Ndogo
mithili ya ndura,
Watu
inowavutia.
68. Nitakupigia debe,
Sitaogopa
wababe,
Nitakata
zao ngebe,
Na
majina kufifia.
69. Magharibi Mashariki,
Huko
nimeshadiriki,
Kukusanya
mashabiki,
Ila
rai wametoa.
70. Wanasema zinga ngata,
Zigo
la miba matata,
Uparani
lachunyuta,
Tatamani
kulitua.
71. Walio kwenye fungate,
Uwageuze
viwete,
Himayani
uwafute,
Mpini
ukishikia.
72. Wabaya siwapakate,
Chemba
nao usitete,
Watakutemea
mate,
Harufu
mbaya katoa.
73. Wenye maneno tutumbi,
Kwako
wasiweke kambi,
Wakaleta
kalimambi,
Mambo
kukuharibia.
74. Na ugeuke mbilimbi,
Kwa
wafanyao vitimbi,
Sijifanye
chakubimbi,
Wakaja
kukuzoea.
75. Siendekeze uchwara,
Ukashindia
kangara,
Yatakupata
madhara,
Utashindwa
kupumua.
76. Watembelee sitimbi,
Ukale
nao magimbi,
Usiogope
mavumbi,
Wa
mjini kajitia.
77. Ufike hadi muhoro,
Ukale
nao uporo,
Kitawaisha
kihoro,
Wewe
watakuchagua.
78. Uende kwa wapogoro,
Ukatishe
vichochoro,
Usiogope
nguchiro,
Usije
kuwakimbia.
79. Kibwaya hadi mkami,
Bwakila
chini Dutumi,
Twende
pamoja na mimi,
Ndugu
kuwatembelea.
80. Twende wote
chumbageni,
Hadi
kule mtendeni,
Tukatishe
forodhani,
Tupite
kusalimia.
81. Twende hadi Msangani,
Kwa
mfipa na simbani,
Mwendapole
uwanjani,
Uma
kuuhutubia.
82. Temeke mikoroshoni,
Ilala
mchikichini,
Hadi
kule Kinondoni,
Yapasa
kuwafikia.
83. Waliokwama shuleni,
Kisa
ada mfukoni,
Wapatie
udhamini,
Elimu
kumalizia.
84. Utumie lako chogo,
Kwa
kubebea mizigo,
Usije
kupata pigo,
Mali
zikaja potea.
85. Uwaheshimu madingi,
Wanajua
ya mtungi,
Usijifanye
shangingi,
Utakuja
kupotea.
86. Bi kirembwe wa
Giningi,
Sijipake
yake rangi,
Utaja
tiwa masingi,
Shingo
kajivunjikia.
87. Fanya sana mazoezi,
Isije
kata pumzi,
Uwakimbizapo
wezi,
Njiani
ukaishia.
88. Uidumishe nidhamu,
Kwa
wake na maghulamu,
Vumilia
chungu tamu,
Ndivyo
ilivyo dunia.
89. Safari hii ni ndefu,
Utupange
safusafu,
Umoja
kama siafu,
Mungu
atatujalia.
90. Usijivike mikufu,
Ukwasi
inoarifu,
Usipende
kujisifu,
Hadhi
utajishushia.
91. Ng’mbo sitege sikio,
Tageuka
jumbe ndio,
Wakafanya
kimbilio,
Vyetu
kuja kuchukua.
92. Mafukara wape shavu,
Waje
pata utulivu,
Uwakomeshe
wavivu,
Shiriki
walokalia.
93. Wachome vichanchede,
Wasage
akina dude,
Muinue
Juma Dede,
Uchumi
kuuinua.
94. Hayo hayakunichosha,
Kwako
ninayafikisha,
Kazi
yangu imeisha,
Wewe
nakutegemea.
95. Nimewalisha limbwata,
Juu
yako wamedata,
Zitapochangwa
karata,
Dume
utaambulia.
96. Kuna jiji nilipita,
Mno
nikafadhaika,
Wenyeji
waponicheka,
Demu
kumpigania.
97. Kaniweka kwenye kiti,
Hoja
zao si thabiti,
Iweje
mwenye matiti,
Cheo
tukumpatia.
98. Wakaniona kituko,
Siwezi
pata mashiko,
Mana
wao kwao mwiko,
Mke
jambo kuamua.
99. Mke akishaolewa,
Wao
wanavyoelewa,
Kazi
yake amepewa,
Mume
kumhudumia.
100. Kweli nilisikitika,
Moyo
ukahuzunika,
Mwili
ukasisimka,
Maneno
nilosikia.
101. Kwanza nilishika
tama,
Na
chini nikainama,
Kisha
ndo nikasimama,
Vikwazo
kuvipangua.
102. Hakuumbwa Mwanamke,
Aje
adharaulike,
Apewe
nafasi yake,
Jamii
kuhudumia.
103. Mwanume si sababu,
Eti
kuwa muhasibu,
Kigezo
ni mahesabu,
Kuweza
kukokotoa.
104. Amekusanya nyaraka,
Kaka
yake ajashika,
Akapewa
mamlaka,
Kuingoza
Dunia.
105. Ninatamka kwa dhati,
Zimepitwa
na wakati,
Mila
zenye mashariti,
Wanawake
kubagua.
106. Tafakari kwa makini,
Mwanamke
si haini,
Haweki
sumu jikoni,
Chungu
tumempatia.
107. Kaacha zote anasa,
Kwa
muda miezi tisa,
Ili
kisa na mkasa,
Uje
iona dunia.
108. Hawezi kuwa dhalimu,
Mtu
huyu maghulamu,
Tumpe
ili jukumu,
Nema
atatuletea.
109. Maswali wakauliza,
Mengi
nikawaeleza,
Wakabaki
wanawaza,
Kama
wapotea njia.
110. Kiukeni kuta hizi,
Muondoe
usingizi,
Ushahidi
huu wazi,
Mwanakwetu
atufaa.
111. Hapo walitahayari,
Baada
ya tafakuri,
Nao
wakawa tayari,
Yeye
kumshangilia.
112. Zikatawala kelele,
Shangwe
na vigelegele,
Mwanakwetu
lele!lele!
Nguvu
tutakupatia.
113. Kazi kwako
Mwanakwetu,
Ewe
kipenzi cha watu,
Nakupigia
upatu,
Funguo
kushikilia.
114. Chozi linanidondoka,
Na
goti ninaanguka,
Mwana
uliyetukuka,
Nyumba
yetu angalia.
115. We fasaha wa fikira,
Njoo
ulete tijara,
Naapa
sitakugura,
Shime
takupigania.
116. Mwanakwetu una hamu,
Kutaka
kunifahamu,
Nisije
fika hatamu,
Kabula
kunitambua.
117. Jina langu ni Lutufu,
Sijiviki
utukufu,
Mimi
kiumbe dhaifu,
Nazidi
kudidimia.
118. Natoka koo ya Mbanga,
Jumbe
mlima mpunga,
Wala
sio mmachinga,
Rufiji
ninatokea.
119. Sihitaji senti yako,
Naitaji
wema wako,
Kwa
hili taifa lako,
Uje
kulihudumia.
120. Kalamu ninaiasi,
Ngoja
nipande farasi,
Kwa
kasikazi na kusi,
Jinalo
kulinadia.
Mtunzi: Lutufu A. Mbanga
(Utu busara)
Simu: 0655-133337
Barua pepe:
lutufumbanga@gmail.com
0 comments:
Post a Comment