mwanazuoni

KINGUNGE AWALILIA MASIKINI KATIKA BUNGE LA KATIBA

Na Magreth Kinabo, Dodoma
Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, ambaye pia ni Mwanasiasa mkongwe, Mzee Kingunge Ngombale  Mwiru ameeleza siri iliyomsukuma  kutoa mapendekezo yake  ya sura mpya juu ya lengo la mageuzi ya maendeleo ya kiuchumi  na kijamii na kujitegemea kuwa ni unyonge wa watu wengi ili waweze kuondokana na umasikini.
 Aidha Mzee  Kingunge ambaye ni mjumbe wa Bunge hilo kutoka kundi la  201 alisema alijifunza katika semina ya Dk. Amos Wako ambaye alikuwa Mwansheria Mkuu wa Kenya   kwamba  ili kuweza kuwa na usawa wa binadamu ni lazima kujali haki za  makundi mbalimbali.
Aliyataja baadhi ya  makundi hayo, kuwa ni wafugaji, wavuvi, wakulima vijana na mengineyo.
“ Haki  zote hizi zilikuwepo katika Katiba ya mwaka 1977 na Katiba za nchi mbalimbali, lakini wanaofaidi  haki  hizo  katika nchi hizo ni wale wenye nacho,” alisema Mzee Kingunge.
Aliongeza kwamba watu wanaishi lakini hawana uhakika wa kuwa na chakula cha kesho.
“ Mimi nimependekeza kwenye Kamati yangu Namba Nane, mawazo yangu yamepelekwa katika Kamati mbalimbali na wengine walelezea vizuri kuliko mimi,” alisema.
Mzee Kingunge alisema  hayo huku akitoa mfano wa Hayati wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius  Nyerere kuwa kilichomsukuma kugombania uhuru ni unyonge wa mwafrika, lakini yeye ni unyonge wa watu wengi.
“Sisi ni waafrika lazima tujitambue Sisi nani…sisi ni watu kama wengine, wenzetu wa Mashariki wameendelea kwa sababu ya  maarifa ya kisasa ya Sayansi  na Teknolojia na sisi maarifa tunayo na sasa hivi tunaweza kuyapata hata ambayo hatuna.
“Ninapendekeza jambo kuu moja kujenga uchumi wa kisasa wa taifalinalojitegemea, maana yake ni tujikite katika maarifa ya kisasa ya Sayansi na Teknolojia,tufanye  mapinduzi bora ya elimu, kilimo, ufugaji, uvuvi ili yawe ya kisasa,” alisisitiza.  
Alisema pili ni kuanzisha mchakato wa mapinduzi ya viwanda,ambayo ni kujenga sekta muhimu za nishati, mawasiliano na miundombinu kwa kuwa yote hayo yanatuelekeza kwenye kujenga taifa linalojitegemea.
Mzee Kingunge alisema ni vema kujenga nchi yenye maendeleo linganifu ya kiuchumi na kijamii katika taifa, uwezeshaji wa wananchi kiuchumi na kijamii, upangaji wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii na kujitegemea, rasilimali za nchi na matumizi yake na utafiti wa maendeleo
“Katika kujenga dhamira ya kujenga uchumi wa kisasa wa taifalinalojitegemea, mafanikio katika jambo yatategemea mambo matatu, ambayo ni wananchi kufanya kazi kwa bidii, kwa maarifa na nidhamu,” alisema.
Alisema kufanya hivyo ni kuwaondoa asilimia 65 ya wakulima wanao tumia jembe la mkono, kuhibiti ufugaji wa kuhamahama na kuhakikisha wana malisho na maji kwa ajili ya mifugo yao jirani na makazi yao.
Aliwataka wajumbe wa Bunge hilo, walisoma ili waweze kufanya maamuzi ya kihistoria.
Alifafanua kuwa umasikini hautaondoka kwa miujiza, bali kwa misingi kama hiyo,  kwa kuwa haki nyingine zinategemea uchumi, huki akitoa mfano China waliweza na kuweka historia.
Share on Google Plus

. Mtani

Mshana is Tanzanian blogger who writes different news without bias, He provides social, political and sports as well as Entertainment news happening in all parts around the World."STAY ME ALL THE TIME FOR INSTANT UPDATES.."
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment