mwanazuoni

HATMAE MHE: BERNARD MEMBE AMJIBU ZITTO KABWE




YAH: FEDHA ZA DENI LA LIBYA
1.0. Libya ni moja kati ya nchi wafadhili wa Tanzania ambapo, kama ilivyo wafadhili wengineimekuwa ikiipa nchi yetu misaada na mikopo yenye masharti nafuu. Serikali yetu imekuwa ikifanya taratibu mbalimbali kulipa madeni ya nchi wafadhili kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na utaratibu wa kubadili madeni na kuyaingiza katika miradi n.k, yaani ‘Dept Swap’
2.0. Katika utaratibu huo wa ‘Dept Swap’, tarehe 20/7/2005, Serikali ya Tanzania na Libya zilitia sahihi mkataba wa Dept Swap (Dept Swap Agreement) ambao uliweka utaratibu wa matumizi na urejeshaji wa fedha za deni la Libya.
3.0. Tarehe 4/3/2009, Serikali ya Libya na Tanzania zilitia sahihi mkataba wa nyongeza (Addendum to the Dept Swap Agreement) ambao ulizungumzia, pamoja na mambo mengine, matumizi ya jumla ya dola za Kimarekani milioni 20 (20,000,000) ambazo zilikuwa zimehifadhiwa katika akaunti ya Libya No.004-200-0002216-01, Benki ya Rasilimali Tanzania (Tanzania Investment Bank).
4.0. Nyongeza hii ya mkataba ilitamka bayana katika kifungu No.4.02, kwamba, fedha zilizokuwa katika akaunti tajwa, zikopeshwe kwa mwekezaji waliyemteua wao wenyewe, ambaye ni kampuni ya MEIS INDUSTRIES LIMITED kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa kiwanda cha Saruji Lindi. Kwa mujibu wa nyongeza hii, mkopo ulipaswa kulipwa ndani ya miaka sita, na baada ya hapo, fedha hizo zirejeshwe na ziendelee kukopeshwa Watanzania kwa ajili ya miradi mingine ambayo Serikali za Libya na Tanzania zitakuwa zimeridhia.
5.0. Kumbukumbu zinaonyesha mambo mawili:-
5.1 Kwamba, kabla ya Serikali ya Libya kutia sahihi nyongeza hii ya mkataba iliyotaka fedha zikopeshwe kwa MEIS INDUSTRIES, upembuzi yakinifu wa mradi husika ulifanywa na serikali ya Libya kupitia vyombo vyake, na wao wenyewe walishajiridhisha juu ya ubora wa mradi huo (Viability of the Project)
5.2 Kwamba, baada ya kutia sahihi nyongeza ya mkataba, Serikali ya Libya kupitia Ubalozi wake hapa nchini iliendelea kusisitiza kwa maandishi kwamba Serikali ya Tanzania iharakishe mchakato wa kuwezesha fedha hizo zikopeshwe kwa mwekezaji waliyemteua ili mradi huo muhimu usiendelee kuchelewa, na pia fedha ziingie katika mzunguko kwa manufaa ya Watanzania.
6.0. Katika kutekeleza mikataba hii miiwli, yaani Dept Swap Agreement ya tarehe 20/7/2005 na Addendum Dept Swap Agreement ya Tarehe 4/3/2009, na kwa kuzingatia umuhimu ambao serikali ya Libya iliuonyesha, Serikali ya Tanzania kupitia watalaamu wake wa Wizara ya Fedha, Benki ya Rasilimali (TIB) na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, na Mwekezaji (Kampuni ya MEIS), walikutana chini ya usimamizi wa Wizara ya Fedha na kuandaa hadidu za rejea ambazo zilipelekea kutengenezwa kwa mkataba wa uwekezaji (Investment Agreement) kati ya serikali ya Tanzania, TIB, Serikali ya Libya na Mwekezaji.
7.0. Serikali ya Tanzania, TIB na Mwekezaji walitia sahihi mkataba huu na kuupeleka Libya ili serikali ya Libya ipate kuweka sahihi. Kwa sababu ambazo hazikufahamika, serikali ya Libya haikutia sahihi mkataba huo.
8.0. Baada ya kufuatilia kwa muda mrefu bila mafanikio, mwekezaji alimuandikia barua Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania yenye kumbukumbu No. PC/MEIS/AG/2/10 ya tarehe 1/9/2010 akieleza kusudio la kuipeleka Serikali ya Libya Mahakamani kwa kitendo chake cha kutokutia sahihi mkataba.
9.0. Terehe 13/9/2010, Mwekezaji alifungua shauri Mahakama Kuu ya Tanzania, shauri la madai No. 124/2010 dhidi ya serikali ya Libya, akiiomba Mahakama Kuu itoe tamko kwamba kitendo cha serikali ya Libya kukataa kutia sahihi mkataba huu hakikuwa kitendo cha haki na kwamba mahakama itoe amri kwamba fedha hizo zitolewe kwa Mwekezaji ili kutekeleza mradi uliokusudiwa. Kumbukumbu zinaonyesha kwamba wito wa Mahakama (Summons) ulipelekwa Ubalozi wa Libya lakini hapakuwa na majibu wala mwakilishi aliyekuja mahakamani.
10.0. Mahakama Kuu, kwa kufuata taratibu zake, iliendelea na kusikiliza shauri na kutoa amri kama ambavyo mahakama yenyewe ilijiridhisha. Amri ya mahakama, pamoja na mambo mengine, iliagiza kwamba fedha hizo zitolewe kwa mwekezaji ili kutekeleza mradi husika.
11.0. Zilifanyika juhudi za Benki ya Rasilimali (TIB) pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupinga au kupata ufafanuzi zaidi juu ya amri hiyo ya utekelezaji wake. Mahakama Kuu pamoja na Mahakama ya Rufana, katika nyakati tofauti, zilishughulikia maombi hayo na kuyafikisha katika hatima yake kwa mujibu wa sheria. Kwa ajili ya kumbukumbu, mashauri yaliyofunguliwa ni kama ifuatavyo:-
11.1 TIB ilifungua maombi No. 126/2010 katika mahakama ya Rufaa kuiomba izuie na kufuta utekelezaji wa amri ya Mahakama Kuu. Maombi haya ya TIB yalifanyiwa uamuzi wa mwisho mnamo tarehe 7/11/2011, ambapo maombi hayo yaliondolewa mahakamani kwa kuwa, kwa mujibu wa Mahakama ya Rufaa, hayakuwa yamefuata taratibu za kisheria.
11.2 Mwanasheria Mkuu wa Serikali naye akapeleka maombi Mahakama ya Rufaa. Maombi ya kwanza, maombi namba 146/2010 akiomba Mahakama ya Rufaa kufuta mwenendo mzima wa kesi pamoja na amri ya Mahakama Kuu, na maombi ya pili No. 147/2010 ikiiomba Mahakama ya Rufaa izuie utekelezaji wa amri ya mahakama Kuu (Stay of Execution). Maombi haya yote yalisikilizwa na kuamuliwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za kimahakama.
12.0 Wakati haya yakiendelea, ilijitokeza kampuni ya Mohamed Enterprises Limited ikidai kwamba ina haki juu ya fedha hizi. Nayo ikafanya yafuatayo:-
12.1 Ilipelea maombi Mahakama Kuu kuzuia utekelezaji wa hukumu kwa madai kuwa kampuni hiyo nayo ilikuwa ikiishtaki Serikali ya Libya katika kesi ya madai No. 110/2010 na kwa hiyo, endapo amri ya Mahakama Kuu ingetekelezwa kwa kumpa mwekezaji (Kampuni ya MEIS) fedha za Libya, basi wao (Mohamed Enterprises Limited) wangekosa mahali pa kutekeleza/kukazia hukumu waliyokuwa wakiitarajia katika kesi yao (no. 110/2010) dhidi ya serikali ya Libya. Maombi haya yalisikilizwa na Mahakama Kuu na kutolewa maamuzi stahiki.
12.2. Kampuni ya Mohamed Enterprises Limited haikuridhika na uamuzi wa Mahakama Kuu kwa hiyo kapeleka shauri hili Mahakama ya Rufaa, kupitia maombi (Civil Revision) No. 2/2011. Maombi haya nayo pia yalisikilizwa na kutolewa maamuzi.
13 Mwisho wa yote maamuzi ya Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa katika mchakato mzima yakawa kwamba mwekezaji (Kampuni ya MEIS) alikuwa na haki ya kupewa fedha za mradi wa Kiwanda cha Saruji Lindi kama ilivyoanishwa katika mkataba kati ya serikali ya Tanzania na Libya. Ni dhahiri kwamba, mgogoro huu ulichujwa na mahakama mpaka ngazi ya juu kabisa, tena kwa nyakati tofauti na mbele ya waheshimiwa majaji wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa.
14.0 Katika Taifa linaloongozwa kikatiba, chini ya utawala wa sheria kama Tanzania, ambapo Mahakama ndicho chombo kilichopewa mamlaka ya mwisho kuamua juu ya haki za raia na hata serikali, si rahisi na wala haitakuwa sahihi kwa mtu yeyote kuhoji uhalali wa mchakato huu kama ulivyoongozwa, kuelekezwa na kuamuliwa na mahakama, isipokuwa tu kama sheria inatoa mwanya mwingine kurudi mahakamani kwa mtu yeyote ambaye hajaridhika au anayetaka kuhoji maamuzi haya kwa namna yoyote.
15. Mahakama iliamua kwa mujibu wa sheria. Na kwa kuwa hakuna aliyeendelea kupinga kimahakama, suala hili lichukuliwe kwamba limefikia mwisho na limefungwa. Lakini hata kiuongozi, na hasa kwa mtu yeyote mwenye kutazama maslahi ya Taifa hili, ni dhahiri kwamba suala la utekelezaji wa mikataba ya kubadilishana madeni ni jambo lenye manufaa kwa Tanzania na linapaswa kila fursa inapojitokeza kutekelezwa haraka. Wenzetu, nchi wafadhili, wanapotoa fursa za kutupunguzia mzigo wa madeni katika utaratibu wenye manufaa kama huu, tutaendelea kuonekana wa ajabu kama tutaendelea kulumbana badala ya kuchangamkia fursa ya maendeleo. Tukwepe mazingira yanayopelekea taifa letu kuonekana kama wale watoto watukutu waliokabidhiwa zawadi ya nyumba, badala ya kuishi kwa shukrani ya nyumba ile, wakagombana na kunyang’anyana fito na kuzitumia kupigana bila kujali kwamba nyumba inaanguka maana fito ndizo zilizo ishikilia.
16.0 Mimi kama Mbunge kutokea Mkoa wa Lindi, na kama Waziri mwenye dhamana ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, nalifuatilia kwa karibu suala hili kwa sababu mbili:-
(i) Kwanza, kuanzishwa kwa mradi huu kutawanufaisha wapiga kura wangu, na Watanzania kwa ujumla kwa kuinua uchumi wetu na kuongeza ajira hasa wa Mikoa ya Kusini ambayo imeachwa nyuma kwa muda mrefu. Utafiti unaonyesha kuwa Mikoa ya Lindi na Mtwara ina utajiri mkubwa wa mali ghafi ya Saruji, na kwa hiyo upo uhakika wa kupata saruji bora na kwa bei nafuu sana.
(ii) Pili, suala hili linagusa mahusiano ya Nchi mbili kwa hiyo lazima Wizara yangu ilisimamie kwa nguvu, umahiri na umakini wote.
17.0 Kama nilivyosema huko nyuma, fedha zote zilizotolewa kwa amri ya Mahakama ni Mkopo. Hazikuchukuliwa kama fedha za EPA au ESCROW. Ni mkopo uliotolewa kwa Kampuni ya MEIS kwa mujibu wa Mkataba wa Makubaliano (Investment Agreement) yenye Masharti Kibenki. Na Masharti hayo ya Kibenki yanamtaka Mwekezaji kuweka dhamana, kulipia riba, kuwekewa muda wa kurudisha mkopo, na anawekewa hatua za kuchukuliwa endapo Mwekezaji huyo atashindwa kulipa mkopo. Kwa lugha nyingine, Kampuni ya MEIS ikishindwa kulipa mkopo huo, itafilisiwa mali zake na TIB itarudishiwa fedha zake. Iacheni benki ifanye kazi yake. Mkopo unageukaje kuwa ufisadi?
18.0 Mimi sina Kampuni hapa nchini. Sina ubia na kampuni yoyote ikiwemo Kampuni ya MEIS. Sina hisa katika Kampuni ya MEIS. Na sijafaidika na mkopo huo ambao unasimamiwa na Benki ya Uwekezaji nchini (TIB). Ndiyo maana uvumi kuwa nahusika na ufisadi wa mabilioni ya Libya hauna mashiko kabisa. Baadhi ya wanasiasa wenzangu wanajua ukweli wote huu lakini kwa makusudi wanaamua kuwafanya watu waamini wapinzani!
19.0 Ujenzi wa kiwanda cha simenti cha Lindi unaendelea vizuri na mitambo yote inayotakiwa katika ujenzi huo imekwisha wasili. Asilimia 45 ya ujenzi wa kiwanda hicho umekamilika na ni mategemeo ya kampuni ya MEIS kuwa kiwanda hicho kitakamilika ifikapo mwezi Disemba mwaka huu wa 2015.
20.0 Ni matumaini yangu kuwa nimeeleweka vya kutosha. Kama kuna mtu anahitaji taarifa zaidi basi awe huru kuihoji kampuni ya MEIS na Benki ya TIB ambayo imetoa mkopo huo, au kumpata Msajili wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa ambazo zote ziliamua Kampuni ya MEIS ipewe mkopo huo kwa mujibu wa sheria za kibenki.
Bernard K. Membe (Mb)
WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA
USHIRIKIANO WA KIMATAIFA



Share on Google Plus

. Mtani

Mshana is Tanzanian blogger who writes different news without bias, He provides social, political and sports as well as Entertainment news happening in all parts around the World."STAY ME ALL THE TIME FOR INSTANT UPDATES.."
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment