mwanazuoni

NATIONAL IDENTITY CARDS INFORMATION TO ALL CITIZENS IN TANZANIA

National Identity Cards Information PDF Print E-mail
1. UTANGULIZI
Wazo la kuanzisha Vitambulisho vya Taifa kwa Raia wa Tanzania na Raia wageni waishio nchini Tanzania lilizaliwa mwaka 1968 katika Kikao cha “Interstate Intelligence Gathering” kilicho-jumuisha wajumbe kutoka nchi za Tanzania, Kenya, Uganda na Zambia. Kwa wakati huo nchi za Kenya na Zambia tayari zilikuwa na Vitambulisho vyao vya Taifa. Iliazimiwa kwamba ili kuimarisha mahusiano ya kiusalama yanayozingatia Utawala wa Sheria katika nchi hizo nne ni lazima nchi za Uganda na Tanzania nazo zikatoa Vitambulisho vya Taifa kwa Raia wao.
Kumekuwa na jitihada mbalimbali za Serikali kuhakikisha Watanzania na wageni wote wanapatiwa Vitambulisho vya Taifa, lakini jitihada hizo hazikuweza kuzaa matunda yaliyotajariwa kwa kipindi kirefu kutokana na sababu mbalimbali. Mwaka 1986 Serikali ilitunga Sheria ya Vitambulisho ambayo haikutumika wala kutungiwa kanuni zake.
Ni ukweli ulio wazi kwamba kwa wakati huu kuna umuhimu mkubwa wa kuwa na Vitambulisho vya Taifa kulingana na mazingira tuliyonayo. Kuanzishwa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo nchi tano zimeungana na kukubaliana kwamba watu wa nchi hizo wanaweza kutembeleana bila bughudha pia kumeongeza umuhimu wa kuwa na Vitambulisho. Ikumbukwe kuwa Tanzania na Uganda ndizo nchi pekee katika Jumuiya hiyo ambazo hazina Vitambulisho vya Taifa.
Upembuzi yakinifu wa Vitambulisho vya Taifa ulikwishafanyika na matokeo ni kwamba Mradi unatekelezeka. Aidha taarifa hiyo imeainisha makadirio ya gharama za Mradi na namna mradi utakavyotekelezwa ambapo teknolojia ya “Smartcard” ndiyo itakayotumika kama ilivyokubaliwa na Baraza la Mawaziri katika kikao kilichokaa mjini Dodoma mwezi Februari, 2007.
Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tayari ametia saini Hati ya kuidhinisha kuanzishwa kwa chombo cha kusimamia Vitambulisho vya Taifa kinachojulikana kama Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa au “National Identification Authority (NIDA)”. Hati hii imechapishwa katika Gazeti la Serikali, GN No.122 ya tarehe 01/08/2008.
Aidha katika Kikao chake cha tarehe 3 Februari, 2007 Baraza la Mawaziri lilitoa mwongozo kuwa iundwe Kamati ya Usimamizi (Steering Committee) ya Makatibu Wakuu, Wakuu wa Idara na Vitengo vinavyohusika na mambo muhimu kuhusu Vitambulisho vya Taifa. Kamati hii pamoja na mambo mengine itakuwa na jukumu la kutoa mwongozo na mwelekeo wa program za Mradi.
Baraza pia liliamua kuwa taarifa ya upembuzi yakinifu ya Kampuni ya Gotham International Limited (GIL) iwe ndio mwongozo wa utekelezaji wa Mradi na Kampuni hiyo iliteuliwa kuwa Mshauri mwelekezi wa Mradi.
Katika hatua nyingine, Serikali ilitoa mwongozo kuwa taarifa mbalimbali za utekelezaji wa mradi ikiwemo ile ya mshindi wa zabuni ya mkandarasi wa kutengeneza mfumo wa Vitambulisho vya Taifa ziwasilishwe katika Baraza la Mawaziri ili kupata ridhaa yake.
2. DHANA YA KITAMBULISHO CHA TAIFA
Swala la mfumo wa Kitambulisho cha Taifa bado ni dhana ngeni miongoni mwa watu wengi hususani umuhimu wake kwa mwananchi, Taasisi mbalimbali na Serikali kwa ujumla. Hata wakati mwingine baadhi ya watu hudhani ya kwamba ni kitambulisho cha Uraia, au ni Kitambulisho kama vilivyo vitambulisho vingine vya kazi, au ni kipande cha karatasi chenye picha, jina la mhusika pamoja na anuani yake.
Dhana nzima ya mfumo wa Kitambulisho cha Taifa ni pana zaidi ya hapo. Pia ni vyema ieleweke kwamba kadi za Vitambulisho vya Taifa zitatolewa kwa watu wazima kuanzia miaka 18 na sio watoto wadogo kama inavyoelezwa.
Vitambulisho vya Taifa kulingana na Nchi mbalimbali mfano Angola, Afrika Kusini, Bostwana na Kenya, ambazo zimeweza kutengeneza Vitambulisho vyao vya Taifa hutengenezwa kutokana na taarifa zilizohifadhiwa kwenye daftari maalum. Daftari hilo hutunza kumbukumbu za mtu kuanzia alipozaliwa hadi mwisho wa uhai wake, huboreshwa kwa kupokea au kuongezwa taarifa za mara kwa mara za mhusika kutokana na matukio mbalimbali yanayomhusu mhusika. Taarifa hizo huhifadhiwa katika daftari moja, na mhusika hukabidhiwa kadi ambayo hutumika kama alama ya utambulisho. Aidha Taasisi nyingine zinaweza kutumia taarifa zilizohifadhiwa kwenye daftari hiyo kwa makubaliano maalum.
Wakati mwingine watu hutaja kitambulisho cha Uraia wakiwa na maana ya Kitambulisho cha Taifa. Ukweli ni kwamba Taasisi hii itahusika na kutengeneza Kitambulisho cha Taifa ambacho kitatolewa kwa Raia wa Tanzaia na watu wengine ambao sio Raia wa Tanzania.
3. UMUHIMU WA MFUMO WA VITAMBULISHO VYA TAIFA
Mfumo wa Kitambulisho cha Taifa unaanzishwa kwa sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na:-
  • Kutambua mtu au mhusika.
  • Kusaidia kumtambua mhusika anapohitaji kupatiwa huduma katika Taasisi mbalimbali mfano benki,taasisi za mikopo, huduma za afya n.k.
  • Kuunganisha mifumo mingine kwa lengo la kuwasiliana na kubadilishana taarifa muhimu ambazo zitalenga kuongeza ufanisi na kupunguza gharama za uendeshaji kuliko ilivyo hivi sasa.
  • Kumtambua mtu pale anapofanya uhalifu wa aina Fulani; hii itasaidia sana katika kupambana na uhalifu.
  •  Kutambua wakwepaji wa kurejesha mikopo kutoka kwenye mabenki hasa pale wakopaji wanapochukua mikopo kutoka katika mabenki mbalimbali.
  • Kuweka kumbukumbu za matukio ya uhalifu katika daftari.
  • Kutambua walipa kodi, hii itasaidia kupambana na wakwepaji wa kulipa kodi.
  • Kumtambua mtu anapofanya biashara mbalimbali kwa kutumia majina tofauti.
  • Kuhakikisha kuwa mtu anapata stahili zake za jamii, kwa mfano kupata malipo ya pensheni, haki za matibabu , haki za kujiunga na shule ikiwa ni pamoja na stahili zozote ambazo Raia wa Tanzania anastahili. Hii itasaidia kuondoa watumishi hewa kwenye “payroll “ ya Serikali.
  • Kuboresha utendaji kazi Serikalini kwa kuwa na kumbukumbu sahihi za watumishi na malipo ya stahili zao; hasa pale wanapostaafu.
  • Kupunguza gharama za mwananchi kutokana na huduma mbalimbali anazozipata kutolewa na Taasisi moja.
  • Kurahisisha zoezi la kuhesabu watu/sensa.
4. MAENEO YANAYOTAKIWA KUBORESHWA ILI KUFANIKISHA MFUMO WA VITAMBULISHO VYA TAIFA
Gharama za kutengeneza Vitambulisho hujumuisha gharama mbalimbali ikiwa ni pamoja na miundombinu yake, rasilimali watu, mafunzo na kuboresha maeneo muhimu yatakayokuwa yakishirikishwa katika utekelezaji wake mfano ni yafuatayo:-
  • RITA (Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini) – kuboresha mfumo wa Usajili wa vizazi na vifo.
  • TRA (Mamlaka ya Kodi) – Uboreshaji wa mfumo wa utoaji wa leseni za uendeshaji wa magari.
  • Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Wizara hii ndiyo msimamizi wa Serikali za Mitaa na ndio wenye taarifa zote za watu Mijini na Vijijini.
  • Polisi, kuboresha mfumo wa taarifa za udhibiti wa uhalifu.
  • Mifumo ya mishahara na ki-utumishi kwa kurahisisha namna ya kuwatambua watumishi.
  • Kuanzisha Mtandao wa Mawasiliano “Networking and Connectivity”.
  • Kujenga vituo vya usajili vya Wilaya (Registration Centres) na kujenga (Data Centre) Makao Makuu.
  •  Kutoa elimu kwa Umma (Public Awareness) ili kuwawezesha kujua umuhimu wa dhana nzima ya Vitambulisho vya Taifa.
  • Kuanza zoezi la usajili wa watu kwa lengo la kupata taarifa muhimu za watu.
  • Taasisi za mifumo ya jamii kama NSSF, PPF, GEPF n.k zitaweza kupata taarifa za watu baada ya kuboresha mifumo yao. Kwa hiyo tunapozungumzia gharama za kuendesha shughuli za Vitambulisho vya Taifa hutumaanishi kadi tu bali ni jumla ya gharama zote za uendeshaji katika kutekeleza zoezi zima la mfumo wa Vitambulisho vya Taifa.
5. HATUA ZA UTEKELEZAJI
Utekelezaji wa Mradi umepangwa kuwa katika awamu mbili ambapo awamu kwanza ni maandalizi ya Mradi na awamu ya pili ni awamu ya utekelezaji wa Mradi wenyewe. Ifuatayo ni taarifa ya utekelezaji wa awamu ya kwanza ya maandalizi ya mradi:-
  • Jengo la ofisi limenunuliwa na kufanyiwa ukarabati pamoja na kuwekewa samani za ofisi
  • Hati ya kuanzisha Mamlaka (Establishment Instrument) tayari imesaniwa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuchapishwa katika Gazeti la Serikali GN. 122 ya tarehe 01/08/2008. Mamlaka hiyo inajulikana kama “National Identification Authority” (NIDA) au Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa
  • Zabuni kwa utaratibu wa Pre- Qualification ilitangazwa na Makampuni 104 yalijitokeza kununua vitabu vya zabuni.
  •  Makampuni 54 yalirudisha zabuni zao
  • Kamati ya Uchambuzi ilitumia mwezi mmoja kufanya tathimini na kupendekeza makampuni manane (8) yaingie katika hatua inayofuata.
  • Bodi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ilikutana na kuridhia mapendekezo ya Kamati ya Uchambuzi.
 
Share on Google Plus

. Mtani

Mshana is Tanzanian blogger who writes different news without bias, He provides social, political and sports as well as Entertainment news happening in all parts around the World."STAY ME ALL THE TIME FOR INSTANT UPDATES.."
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment